NGUVU ZA BWANA

David Wilkerson (1931-2011)

Roho Mtakatifu aliniongoza kusoma Kutoka 12, ambayo ina simulizi la ukombozi wa Israeli kutoka Misri.

Kwenye mlango wa kila nyumba ya Waisraeli, damu ya mwana-kondoo iliwekwa kwenye miimo miwili ya kando na kizingiti cha juu. Hii ilikuwa ni kuwalinda watu wa Mungu dhidi ya malaika wa kifo anayepita. Siku ilipofika, umati wa Waisraeli ulitoka utekwani, wanaume wapatao 600,000 pamoja na wanawake na watoto. “…Ikawa kwamba majeshi yote ya Bwana yalitoka katika nchi ya Misri” (Kutoka 12:41).

Katika sura iliyofuata, nilisimama kwenye mstari unaosomeka, “Ikumbuke siku hii uliyotoka Misri, katika nyumba ya utumwa; kwa kuwa Bwana aliwatoa mahali hapa kwa nguvu za mkono wake” (Kutoka 13:3). Watu wa Mungu waliokolewa kwa nguvu za Bwana pekee!

Daudi anatangaza hivi: “Mungu ni nguvu zangu na uweza wangu, naye huimaliza njia yangu…. Alipeleka kutoka juu, akanishika, akanitoa katika maji mengi. Aliniokoa na adui yangu mwenye nguvu, kutoka kwa wale walionichukia; maana walikuwa na nguvu kunishinda…. Naye Mungu, njia yake ni kamilifu; neno la Bwana limethibitishwa; yeye ni ngao yao wote wanaomtumaini” (2 Samweli 22:33,17-18, 31).

Imani na nguvu zetu zinaweza kudhoofika, lakini nyakati zetu za udhaifu, Mungu ametupa ahadi za ajabu za kutufanya upya na kututia nguvu.

  • “Wale waliojikwaa wamejivika nguvu” (1 Samweli 2:4).

  • “Bwana atawapa watu wake nguvu; Bwana atawabariki watu wake kwa amani” (Zaburi 29:11).

  • “Mungu wa Israeli ndiye awapaye watu wake nguvu na uweza. Mungu asifiwe!” ( Zaburi 68:35).

  • “Usinitupe wakati wa uzee; usiniache nguvu zangu zipungukapo… nitakwenda kwa nguvu za Bwana MUNGU; Nitaitaja haki yako, yako peke yako” (Zaburi 71:9,16).

Mpendwa, unaamini Mungu wetu ana nguvu? Ikiwa ana nguvu, hakuna nguvu inayoweza kusimama mbele yake. Kwa hiyo, weka kila kitu katika mkono wake mkuu wa nguvu na uweza. Atafanya njia. Zaidi ya yote, amini neno hili: “Siku ile nilipolia, ulinijibu, na kunitia moyo kwa nguvu nafsini mwangu” (Zaburi 138:3).

Mungu akupende na akubariki.